Friday, February 8, 2013

ALLAH HATAZAMI MIILI WALA SURA, BALI ANATAZAMA NYOYONI

Hadiyth Ya 1, Katika kitabu cha Hadithi za Mtume (s.a.w.): LU-ULU-UN MANTHUWRUN

عَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ (رضي الله عنه)  قَالَ: قَالَ رَسُولُ اللَّهِ  (صلى الله عليه و آله وسلم): ((إِنَّ اللَّهَ لاَ يَنْظُرُ إِلى أجْسَامِكُمْ  وَلاَ إِلَى صُوَرِكُمْ وَلَكِنْ يَنْظُرُ إِلَى قُلُوبِكُمْ)) رواه مسلم 

Imepokelewa kutoka kwa Abu Hurayrah (رضي الله عنه) amesema: Mtume (صلى الله عليه وآله وسلم) amesema: ((Hakika Allaah Hatazami viwiliwili vyenu wala sura zenu, lakini Anatazama nyoyo zenu)).[1]

Mafunzo Na Hidaaya:

  1. Umuhimu wa kuwa na niyyah safi na ikhlaasw katika kumuabudu Allaah (سبحانه وتعالى) kwani hivyo ndivyo tulivyoamrishwa:

وَمَا أُمِرُوا إِلَّا لِيَعْبُدُوا اللَّـهَ مُخْلِصِينَ لَهُ الدِّينَ حُنَفَاءَ وَيُقِيمُوا الصَّلَاةَ وَيُؤْتُوا الزَّكَاةَ ۚ وَذَٰلِكَ دِينُ الْقَيِّمَةِ   

((Na hawakuamrishwa ila kumwabudu Allaah kwa kumtakasia Dini, hunafaa [wakielemea Dini ya haki na kuacha Dini potofu] na wasimamishe Swalaah, na watoe Zakaah, na hiyo ndiyo Dini iliyo sawa)).[2]

  1. Hima ya kutenda ‘amali njema baada ya kuwa na  niyyah safi.

  1. ‘Amali na ‘Ibaadah hazipokelewi isipokuwa niyyah ikiwa ni safi kwa ajili ya Allaah (سبحانه وتعالى) [Al-Kahf 18: 103-104, 110, Al-Furqaan 25: 23].

  1. Hakuna ajuaye yaliyo moyoni mwa mja isipokuwa Allaah (سبحانه وتعالى) [Al-Mulk 67: 13, Huwd 11: 5, Faatwir 35: 38, Al-Hadiyd 57: 6, At-Taghaabun 64: 4].

يَعْلَمُ خَائِنَةَ الْأَعْيُنِ وَمَا تُخْفِي الصُّدُورُ 

 (([Allaah] Anajua hiyana ya macho na yanayoficha vifua)).[3]

  1. Binaadamu hawezi kuficha kitu kwa Allaah, kwani ‘amali na siri zote zitadhihirika Siku ya Qiyaamah. [Aal-‘Imraan 3: 29, Az-Zumar 39: 7, Al-An’aam 6: 60, At-Tawbah: 94, Al-Jumu’ah 62: 8, Atw-Twaariq 86: 9].

  1. Ni muhimu kwa Muislamu kuzitekeleza amri za Dini yake na si kwa mandhari pekee. Na mara nyingi watu huwa ni wenye kusema pindi anapotenda jambo ovu kuwa: “Lakini niyyah yangu ni nzuri”. Hapa Muislamu anatakiwa aizingatie Hadiyth nyengine inayosema: ((Hakika Allaah Hatazami viwiliwili vyenu wala sura zenu, lakini Anatazama nyoyo na ‘amali zenu)).[4] Hivyo, ‘amali zinafaa ziende sambamba na Aliyoyateremsha Allaah na kuja nayo Mtume wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم).

  1. Usimhukumu mtu kwa mandhari yake, pindi ukimuona mtu shakili yake na hakuvaa mavazi ya Muumin ukadhania ni mtu muovu, huenda akawa ni mwema. Hali kadhalika, pindi ukimuona mtu shakili yake na mavazi yake ni ya ki-Muumin ukadhani kuwa ni mtu mwema kabisa, lakini huenda akawa ni mtu muovu.

  1. Kuzingatia yanayomridhisha Allaah (سبحانه وتعالى) daima.

1 Muslim
2 Al-Bayyinah (98:5)
3 Ghaafir (40:19)
4 Muslim

No comments: