Tuesday, July 30, 2013

MASIKU YA KUMI LA MWISHO LA MWEZI WA RAMADHAN


Masiku ya kumi la mwisho la mwezi mtukufu wa Ramadhani, yana fadhila na khususia nyingi kathiri, miongoni mwake ni pamoja na kwamba:
i. Ndani ya masiku hayo umo usiku wa cheo/heshima, ambao huo ni bora kuliko miezi alfu moja. Na ye yote atakaye simama kufanya ibada katika usiku huo, kwa kumuamini Allah kikweli na kwa kutaraji ujira kutoka kwake, huyo atasamehewa dhambi alizokwisha zitenda.

ii. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alikuwa akijitahidi sana kufanya amali ndani ya masiku hayo kuliko siku nyingine. Kama alivyosema Bi. Aysha-Allah amuwiye radhi-alikuwa akiyahuisha masiku haya kwa kusoma Qur-ani, kuleta dhikri, kuswali na kuomba dua halafu ndipo hula daku. [Rejea SAHIH MUSLIM]
iii. Mtume-Rehema na Amani zimshukie-alikuwa linapoingia kumi la mwisho, hufunga kibwebwe (yaani hujitenga na wakeze ili apate faragha ya ibada). Akauhuisha usiku wake na akawaamsha wakeze kufanya ibada pamoja nae. Mtume alikuwa akisimama kufanya ibada katika kumi hili bila ya kulala, zoezi hili hakupata kulifanya katika masiku mengine. Alikuwa akifanya hivyo kwa lengo la kuvuna ujira unaobubujishwa ndani ya masiku hayo na kuiwania Laylatul-Qadri.
iv. Katika jumla  ya khususia (mambo pweke yapatikanayo humo) ni kwamba Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alikuwa akikaa itikafu msikitini ndani ya kumi lote hili la mwisho bila ya kutoka ila kwa haja/dharura kuu.

Fadhila/ubora wa Laylatul-Qadri:
          Allah Taala ameujaalia usiku huu kuwa ndio bora ya masiku yote na akautaja vema katika kitabu chake kitukufu, akasema: "HAKIKA TUMEKITEREMSHA (kitabu hicho) KATIKA USIKU ULIOBARIKIWA. HAKIKA SISI NI WAONYAJI. KATIKA USIKU HUU HUBAINISHWA KILA JAMBO LA HIKIMA". [44:3-4] Usiku mbarikiwa unaotajwa na aya hii ni usiku wa Laylatul-Qadri upatikanao ndani ya mwezi mtukufu wa Ramadhani. Usiku huu umebarikiwa kwa sababu ya kheri, baraka na fadhila zipatikanazo humo. Na katika jumla ya baraka za usiku huo ni kushushwa kwa Qur-ani Tukufu ndani yake. Halafu tena Allah Taala akausifia usiku huo kwamba linabainishwa ndani yake kila jambo la hekima. Yaani mambo hupambanuliwa na kugurishwa kutoka katika "Lauhul-Mahfuudh" uliohifadhi mambo yote hapo. Wakapewa malaika waandishi kuandika mambo yote yatakayotokea ndani ya mwaka mzima, tokea masuala ya riziki, vifo na kadhalika.
Na katika kuonyesha ubora wa usiku huu, Allah Taala ameshusha sura nzima kwa jina la usiku huu, sura inayosomwa mpaka siku ya Kiyama, akasema: "HAKIKA SISI TUMEITEREMSHA QUR-ANI KATIKA LAYLATUL-QADRI; USIKU WA CHEO KITUKUFU. NA NINI KITAKACHO KUJULISHA NINI LAYLATUL-QADRI? LAYLATUL-QADRI NI BORA KULIKO MIEZI ELFU. HUTEREMKA MALAIKA NA ROHO KATIKA USIKU HUO KWA IDHINI YA MOLA WAO MLEZI KWA KILA JAMBO. AMANI USIKU HUO MPAKA MAPAMBAZUKO YA ALFAJIRI". [97:1-5] Allah akazitaja fadhila za usiku huu ndani ya sura hii, kwamba:
i. Huo ndio usiku ulimoshushwa ndani yake Qur-ani Tukufu kwa ajili ya kuwaongoza wanadamu.
ii. Huo ni usiku bora kuliko miezi elfu moja (miaka themanini na tatu).
iii. Malaika hushuka ndani ya usiku huo wakileta kheri, baraka na rehema za Allah kwa waja wake.
iv. Usiku huo ni usiku wa amani tupu. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-amesema kuhusiana na usiku huu mtukufu: "Atakayesimama (kufanya ibada katika) usiku (wa) Laylatul-Qadri, kwa imani na kutarajia ujira kutoka kwa Allah. Atasamehewa dhambi zake zilizotangulia". Bukhaariy & Muslim-Allah awarehemu.
Wakati wa Laylatul-Qadri:
          Usiku huu mtukufu wa Laylatul-Qadri unapatikana ndani ya mwezi mtukufu wa Ramadhani kila mwaka mpaka kusimama kwa Kiyama. Umo ndani ya kumi la mwisho la mwezi huu na hutarajiwa zaidi katika nyusiku za witri; yaani mwezi 21, 23, 24, 25 ,27 na 29. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-amesema: "Izengeeni Laylatul-Qadri katika kumi la mwisho la Ramadhani". Bukhaariy-Allah amrehemu.
Na katika hilo kumi la mwisho, inatarajiwa zaidi kupatikana ndani ya mwezi ishirini na saba, hili ni kwa mujibu wa kauli ya Mtume-Rehema na Amani zimshukie: "...Basi ye yote atakaye kuizengea na aizengee katika saba ya mwisho". Bukhaariy & Muslim-Allah awarehemu.
Allah Taala ametufichia kujua usiku maalumu wa Laylatul-Qadri kwa ajili ya kutuonea rehema ili tukithirishe amali njema katika kuutafuta. Na kwa kufanya hivyo, mja huzidi kuwa karibu mno na Mola wake. Na kumesuniwa katika usiku huu wenye baraka, kukithirisha dua na dua njema ya kuombwa ndani yake ni ile Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-aliyo mfundisha mkewe; Bi. Aysha-Allah amuwiye radhi: "ALLAAHUMMA INNAKA `AFUWUN TUHIBBUL-`AFWAA FA'AFU `ANNAA". Tirmidhiy-Allah amrehemu.

Source : http://www.uislamu.org/nasaha/ramadhani6.htm

No comments: