Wednesday, August 7, 2013

MAMBO MATATU YANAYOFUATIA RAMADHAN


Zakaatul-Fitwr, 'Iydul-Fitwr Na Swawm Ya Sittatush Shawwaal

Tunakaribia kumaliza mwezi Mtukufu wa Ramadhaan na mambo matatu yafuatayo ya muhimu yanayotukabili yanapasa kuzingatiwa ili tukamilishe Swawm zetu ipasavyo na tupate fadhila zake.

1- ZAKAATUL-FITWR  
Inaitwa Zakaatul-Fitwr (Zakaah ya Kufuturu au Kufutari) kutokana na kumalizika Swawm ya Ramadhaan. Imefaridhiwa mwaka wa pili wa Hijrah katika mwezi wa Ramadhaan. 
Hikmah Yake
Ni kutwaharisha Swawm ya Muislamu kutokana na maneno machafu, ya upuuzi wakati alipokuwa amefunga kwa kulisha maskini chakula ili nao wapate chakula kizuri siku ya ‘Iyd.

 
Ndio maana kutolewa kwake kunakuwa kabla ya kuswali Swalaah ya ‘Iydul-Fitwr. Dalili ifuatayo inathibitisha:
عَنْ ابْنِ عَبَّاس ٍقَالَ فَرَضَ رَسُولُ اللَّهِ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ زَكَاةَ الْفِطْرِ طُهْرَةً لِلصَّائِمِ مِنْ اللَّغْوِ وَالرَّفَثِ وَطُعْمَةً لِلْمَسَاكِينِ مَنْ أَدَّاهَا قَبْلَ الصَّلاةِ فَهِيَ زَكَاةٌ مَقْبُولَةٌ وَمَنْ أَدَّاهَا بَعْدَ الصَّلاةِ فَهِيَ صَدَقَةٌ مِنْ الصَّدَقَاتِ . " رواه أبو داود  بِإِسْنَادٍ حَسَنٍ .

Kutoka Ibn ‘Abbaas (Radhiya Allaahu ‘anhuma) ambaye amesema: “Mtume amefaridhisha Zakaatul-Fitwr kuwa ni twahaara ya mwenye kufunga kutokana na maneno ya upuuzi na machafu, na kulisha masikini. Atakayeitoa kabla ya Swalah basi hiyo ni Zakaah iliyotakabaliwa, na atakayeitoa baada ya Swalah basi hiyo ni miongoni mwa sadaka” [Abu Daawuud kwa isnaad iliyo nzuri].
Na ndio kusudio ya kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala)
((قَدْ أَفْلَحَ مَن تَزَكَّى))   ((وَذَكَرَ اسْمَ رَبِّهِ فَصَلَّى))
((Hakika amekwishafanikiwa aliyejitakasa)) ((Na akakumbuka jina la Mola wake Mlezi, na akaswali)) [Al-A’laa: 14-15]

‘Umar bin ‘Abdul-Aziyz alikuwa akiamrisha watu kutoa Zakatul-Fitwr na huku akisoma Aayah hizo tukufu. 

Wakati Unaowajibika Kutoa
Kuanzia Magharibi ya siku ya mwisho ya Ramadhaan hadi asubuhi kabla ya Swalah ya ‘Iydul-Fitwr. Inaweza pia kutolewa siku mbili tatu kabla. Mtoto atakayezaliwa siku hiyo kabla ya kuzama jua imewajibika kutolewa Zakaatul-Fitwr.

Anayewajibika Kutoa Zakaatul-Fitwr Na Kitu Gani Cha Kutoa
 عَنْ ابْنِ عُمَرَ رَضِيَ اللَّهُ عَنْهُمَا قَال فَرَضَ رَسُولُ اللَّهِ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ زَكَاةَ الْفِطْرِ صَاعًا مِنْ تَمْرٍ أَوْ صَاعًا مِنْ شَعِيرٍ عَلَى الْعَبْدِ وَالْحُرِّ وَالذَّكَرِ وَالأُنْثَى وَالصَّغِيرِ وَالْكَبِيرِ مِنْ الْمُسْلِمِينَ وَأَمَرَ بِهَا أَنْ تُؤَدَّى قَبْلَ خُرُوجِ النَّاسِ إِلَى الصَّلاةِ . صحيح البخاري   

Kutoka kwa Ibn 'Umar (Radhiya Allaahu 'anhuma): "Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ameifanya Zakaatul-Fitwr ni fardhi kwa mtumwa na aliye huru, mwanamume na mwanamke, mdogo na mkubwa miongoni mwa Waislamu kwa kutoa swaa'* moja ya tende kavu au swaa’ moja ya shayiri, na akaamrisha kwamba itolewe kabla ya watu kwenda kuswali (Swalaatul-'Iyd)" [Al-Bukhaariy] 

  • swaa’ moja = kilo mbili na nusu hadi tatu au (mteko) viganja viwili vya mkono vya mtu wa wastani vilivyojaa mara nne.


Kinachotolewa Ni Chakula Kinachotumika Na Watu Katika Nchi:

عن  أبي سَعِيدٍ الْخُدْرِيَّ رَضِيَ اللَّهُ عَنْهُ قَالَ "ُكُنَّا نُعْطِيهَا فِي زَمَانِ النَّبِيِّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ صَاعًا مِنْ طَعَامٍ أو صَاعاً من الشعير, أو صاعاً من تَمر, أو صاعاً من زَبيب، أو صاعاً من أقِط    البخاري  
Abu Sa'iydil-Khudriyy (Radhiya Allaahu 'anhu) amesema: "Tulikuwa tukitoa zama za Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) swaa’ moja ya chakula, au swaa’ ya shayiri au swaa’ ya tende au swaa’ ya zabibu au swaa’ ya aqit" (mtindi mkavu) (ambacho ndicho kilichokuwa chakula chao zama za hizo) [Al-Bukhaariy Na Muslim]
Tafadhali bonyeza kiungo kifuatacho  kuhusu mas-alah mbali mbali ya Zakaatul-Fitwr:

2- ‘IYDUL-FITWR  
Inaitwa ‘Iydul-Fitwr (‘Iyd ya kufuturu au kufutari) kutokana na Waislamu kumaliza funga ya Ramadhaan. Hivyo haifai kufunga Swawm siku ya ‘Iyd, bali ni sikukuu ya Waislamu ya kusherehekea, kufurahi kwa kila njia zilizomo katika mipaka ya Dini.

a)  Apasayo Kufanya Muislamu Yaliyo Sunnah
Kuoga Kabla Ya Kutoka Kwenda Kuswali
فقد صح في الموطأ وغيره أَنَّ عَبْدَ اللَّهِ بْنَ عُمَرَ كَانَ يَغْتَسِلُ يَوْمَ الْفِطْرِ قَبْلَ أَنْ يَغْدُوَ إِلَى الْمُصَلَّى
Imethibitika katika Muwattwaa na vitabu vinginevyo kwamba ‘Abdullaah bin ‘Umar (Radhiya Allaahu ‘anhuma) alikuwa akioga siku ya ‘Iydul-Fitwr kabla ya kwenda Muswallaa.

Kujipamba Na Kuvaa Nguo Nzuri
وعن جابر رضي الله عنه قال : كان للنبي صلى الله عليه وسلم جبة يلبسها للعيدين ويوم الجمعة . صحيح ابن خزيمة   
Kutoka kwa Jaabir (Radhiya Allaahu ‘anhu) ambaye amesema: “Mtume alikuwa ana jubbah akilivaa siku za ‘Iyd mbili na siku ya Ijumaa” [Swahiyh Ibn Khuzaymah]    
Na Ibn ‘Umar (Radhiya Allaahu ‘anhuma) alikuwa akivaa nguo zake nzuri kabisa siku ya ‘Iyd.
Kwa hiyo inapasa kujipamba kwa nguo nzuri, na manukato mazuri. Ama wanawake hawapasi kujipamba na kudhihirisha mapambo yao ikiwa ni mavazi au kujipaka vipodozi na pia hawapaswi kujitia manukato na kutoka nje. Wanaweza kudhihirisha yote hayo mbele ya Maharimu zao tu.


Kula Tende Kabla Ya Kutoka Kwenda Kuswali

عَنْ أَنَسِ بْنِ مَالِكٍ قَالَ كَانَ رَسُولُ اللَّهِ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ لا يَغْدُو يَوْمَ الْفِطْرِ حَتَّى يَأْكُلَ تَمَرَاتٍ .. وَيَأْكُلُهُنَّ وِتْرًا . البخاري  
Kutoka kwa Anas bin Maalik (Radhiya Allaahu ‘anhu) ambaye amesema: “Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa hatoki kwenda kuswali Swalah ya ‘Iyd ila baada ya kula tende… na akila kwa hesabu ya witr. [Al-Bukhaariy]
Hii ni kwa sababu haifai kufunga siku hii ya ‘Iyd. Asiyepata tende anaweza kula kitu chochote.
Ama katika 'Iydul-Adhwhaa ni Sunnah kutokula kabla ya kwenda Msikitini, na anaposhuka baada ya Swalah ni bora kitu cha kwanza kula ni ile nyama ya Udhwhiyah (mnyama aliyechinjwa) ikiwa itapatikana.


Kuleta Takbiyrah Kwa Sauti

Sunnah kuu katika ‘Iyd kutokana na kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):

((وَلِتُكْمِلُواْ الْعِدَّةَ وَلِتُكَبِّرُواْ اللّهَ عَلَى مَا هَدَاكُمْ وَلَعَلَّكُمْ تَشْكُرُونَ ((
((na mtimize hiyo hisabu, na mumtukuze Allaah kwa kuwa Amekuongoeni ili mpate kushukuru)) [Al-Baqarah: 185]

Pia Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akileta Takbirah mpaka anamaliza Swalah. [Silsilat Al-Ahadiyth As-Swahiyhah - Shaykh Al-Albaaniy]

Matamshi Ya Takbiyrah
الله أكبر الله أكبر لا إله إلا الله والله أكبر الله أكبر ولله الحمد
Allaahu Akbar Allaahu Akbar, Laa Ilaaha Illa Allaah, WAllaahu Akbar Allaahu Akbar wa Lillaahil Hamdu  

Wakati wa Takbiyrah

Unaanza usiku wa ‘Iyd mpaka anapoingia Imaam kuswalisha Swalah ya ‘Iyd

Kupongezana

Ni vizuri kupongezana siku ya ‘Iyd baina ya Waislamu, kuzidisha mapenzi baina yao. Na ilivyo Sunnah ni kusema kama walivyokuwa wakiambiana Maswahaba wanapokutana siku ya ‘Iyd ni kusema:
'Tuqubbila Minna wa Minka’ au ‘Taqabbala Allaahu Minnaa wa Minkum’.

Kuelekea Katika Muswallaa Kwa kutembea Na Kurudi Kwa Njia Nyingine
  
عَنْ جَابِرِ بْنِ عَبْدِ اللَّهِ رَضِيَ اللَّهُ عَنْهُمَا قَالَ كَانَ النَّبِيُّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ إِذَا كَانَ يَوْمُ عِيدٍ خَالَفَ الطَّرِيقَ . رواه البخاري    

Kutoka kwa Jaabir bin ‘Abdillaah (Radhiya Allaahu ‘anhuma) ambaye amesema: “Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) alikuwa akibadilisha njia siku ya ‘Iyd” [Al-Bukhaariy]

Hikmah yake ni kwamba njia hiyo itashuhudia siku ya Qiyaamah na ardhi itazungumza yote ya kheri na shari anayotembelea mja juu yake. Pia kudhihirsiha Uislamu katika njia mbili, pia kukutana na watu tofauti na kuwasaidia kwa njia yoyote.


Kuswali Swalah ya ‘Iyd Katika Muswallaa
Ni Sunnah bali, ni waajib kwani Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) aliamrisha watu wote watoke kwenda kuswali:

 عَنْ أُمِّ عَطِيَّةَ رضي الله عنها قَالَتْ "أَمَرَنَا تَعْنِي النَّبِيَّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ أَنْ نُخْرِجَ فِي الْعِيدَيْنِ الْعَوَاتِقَ وَذَوَاتِ الْخُدُورِ وَأَمَرَ الْحُيَّضَ أَنْ يَعْتَزِلْنَ مُصَلَّى الْمُسْلِمِينَ"  مسلم
Kutoka kwa Ummu ‘Atwiyyah (Radhiya Allaahu ‘anhaa) kwamba: “Ametuamrisha Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) tutoke katika ‘Iyd mbili vijana na vikongwe na kaamrisha wanawake wenye hedhi wajitenge katika Muswallaa” [Muslim]

b)  Yaliyo Bid’ah Katika ‘Iyd
Kuleta Takbiyrah Kwa Pamoja Katika Misikiti Na Muswallaa
Inavyopasa ni kila mtu kuleta Takbiyrah pekee.

Kutembelea Makaburi 
Imekuwa ni ada ya baadhi ya watu kutembelea makuburi siku za ‘Iyd. Jambo hili halikufanywa na Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) wala Maswahaba zake. Mtu anaweza uzuru makaburi siku yoyote na si kutenga siku ya ‘Iyd kwa jambo hilo na hadi kugeuka kuwa ni katika Sunnah za ‘Iyd hivi leo.

Maamkizi Ya Kuiga Makafiri
Kupelekeana kadi na zawadi kama wafanyavyo makafiri, haipasi kuwaiga kwani ni jambo tulilokatazwa katika dini na tuwe na fakhari na mila na desturí zetu.

c)  Yaliyo Maasi
Kunyoa Ndevu
Kunyoa ndevu hasa kwa makusudi ya kukusudia ‘Iyd kwa kudhani mtu anapendeza akifanya hivyo ilihali anavunja shari'ah na kupingana na Sunnah za Mtume wetu Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam).

Wanawake Kutokutimiza Hijaab zao za kishari'ah na kudhihirisha mapambo yao mbele ya wasio Maharimu wao.

Sherehe Za Maasi
Kuchanganyika wanawake na wanaume (party) na kuwekwa muziki, vyakula na vinywaji vya haraam na kupeana mikono wanawake na wanaume.
((لأَنْ يُطْعَنَ فِي رَأْسِ أَحَدِكُمْ بِمِخْيَطٍ مِنْ حَدِيدٍ خَيْرٌ لَهُ مِنْ أَنْ يَمَسَّ امْرَأَةً لا تَحِلُّ لَهُ))
Mtume (swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:
“Ni bora kwa mwanaume kupigwa sindano katika kichwa chake kuliko kuushika mkono wa mwanamke ambaye si halali yake.” [Silsilat Al-Ahadiyth As-Swahiyhah - Shaykh Al-Albaaniy] 
Wanawake wanaruhusiwa kuimba Nashiyd siku za ‘Iyd wakiwa peke yao au mbele za Maharimu wao.

Kufanya Israaf ya chakula na mali badala ya kuwasaidia masikini na mafakiri


3- SWAWM YA SITATUSH SHAWWAAL   
Swawm hii inafuatia moja kwa moja baada ya mwezi wa Ramadhaan na siku ya 'Iyd ul Fitr. Ni Sunnah iliyo na fadhila kuu kwani thawabu zake ni sawa na thawabu za mtu kufunga mwake mzima kama alivyosema Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)
(( من صام رمضان ثم أتبعه ستًّا من شوال كان كصيام الدهر)) أرجه مسلم في صحيحه،

((Atakayefunga Ramadhaan kisha akafuatiliza na siku sita za mwezi wa Shawwaal itakuwa kama ni funga ya mwaka)) [Muslim]

Hesabu ya kuwa mwaka mzima ni kutokana na kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):
((مَن جَاء بِالْحَسَنَةِ فَلَهُ عَشْرُ أَمْثَالِهَا وَمَن جَاء بِالسَّيِّئَةِ فَلاَ يُجْزَى إِلاَّ مِثْلَهَا وَهُمْ لاَ يُظْلَمُون))

((Afanyae wema atalipwa mfano wake mara kumi. na afanyae ubaya hatalipwa ila sawa nao tu. Na wao hawatadhulumiwa)) [Al-An'aam:160]

Na kauli ya Mtume Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam):
((إن الله كتب الحسنات والسيئات , ثم بين ذلك , فمن هم بحسنة فلم يعملها كتبها الله له عنده حسنة كاملة فإن هو هم بها فعملها كتبها الله له عنده عشر حسنات , إلى سبعمائة ضعف , إلى أضعاف كثيرة , ومن هم بسيئة فلم يعملها , كتبها الله عنده حسنة كاملة , فإن هو هم بها فعملها كتبها الله له سيئة واحدة )) متفق عليه ،

((Allaah Ameandika mema na mabaya. Kisha Akayabainisha. Basi atakayetia nia kutenda jema kisha asilifanye, ataandikiwa jema moja kamili. Atakapofanya hima na akalitenda, ataandikiwa mema kumi hadi kuzidi mia saba na ziada nyingi. Na atakayetia nia kufanya kitendo kibaya kisha asikifanye, ataandikiwa jema moja kamili. Atakapokifanya  ataandikiwa dhambi moja)) [Al-Bukhaariy ya Muslim]

Maulamaa wanachambua sababu ya kulipwa mja ujira wa mwaka mzima kwa atakayefunga Ramadhaan na siku sita hizo za Shawwaal, kwa kusema: Jambo zuri hulipwa ujira mara kumi, kwa hiyo mtu akifunga siku 30 za Ramadhaan atapata ujira mara kumi; nazo zitakuwa 300, ukijumlisha na siku sita za Shawwaal ambazo zikilipwa mara kumi, huwa 60. Kwa hivyo 300 + 60 = 360, mtu atapata hesabu ya mwaka mzima.
Kwa mantiki hii, tunaona kuna umuhimu na ubora mkubwa wa kuifunga Swawm hii ndugu zangu.


Tunawaombea Waislamu wote wajaaliwe kumaliza mwezi Mtukufu wa Ramadhaan kwa kheri na mafanikio, watakabaliwe Swawm zao, na madhambi kughufuriwa, waweze kutoa Zakaatul-Fitwr za kutakasa Swawm, Wawe na ‘Iyd ya furaha na uwezo wa kufunga Sitatush Shawwaal.
Taqabballa Allaahu Minna wa Minkum

Kwa msaada wa: www.alhidaaya.com

No comments: